photo tyyyyyyyyyyyyyyyy_zpsd20272cf.jpg

CHADEMA WAMLIPUA MWAKYEMBE.

MWENYEKITI wa Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), Mkoa wa Iringa Joseph Lyata, amemlipua Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe kuwa ni mbabaishaji na kuwataka wananchi wa Kyela kumng’oa katika uchaguzi mkuu ujao.
 
Alisema Dk. Mwakyembe ni kigeugeu, kwani yuko tayari kuyakana hata mawazo yake na kutolea mfano kuwa, mbunge huyo ni muumini wa Serikali tatu, lakini ulipofika wakati wa kujadili rasimu ya Katiba, aliyakana mawazo yake jambo ambalo ni hatari kwa kiongozi wa aina hiyo, kwani ipo siku anaweza kuwauza wananchi wake.

Aliongeza kuwa, mbali na kujipambanua kuwa ni mpiganaji wa vita dhidi ya ufisadi ni vigumu kwa kiongozi huyo kufanikiwa, kwani asilimia kubwa ya watu wanaofanya ufisadi katika wizara yake ndiyo wafadhili wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Lyata, alisema Dk. Mwakyembe kamwe haiwezi Wizara ya Uchukukuzi, kwani vitengo vyote vimeshikiliwa na wakubwa ambao sehemu kubwa ndiyo wafadhili wa CCM inayounda Serikali anayoiongoza.

“Dk. Mwakyembe alikuja na kasi ya ajabu, alianza na viwanja vya ndege, ameona kwa moto, akageukia Bandari nako kuchungu, alipojaribu kugeukia reli kumbe kule nako ni hatari, hivyo ni vigumu kwa waziri huyo kufanikiwa.

 Dawa ni kumuondoa katika uchaguzi ujao,” alisema Lyata.

Alisema sifa anayopewa Dk. Mwakyembe, haifanani na haiba aliyonayo, kwani amekuwa akipewa sifa kama kiongozi mpiganaji wakati ni kigeugeu.

Alisema Wilaya hiyo ina miundombinu mibovu wakati Waziri Mwakyembe anahusika na barabara, lakini ameshindwa kuboresha za jimboni kwake.

Katika hatua nyingine, viongozi hao wa BAVICHA walisema wanasikitishwa na hatua ya baadhi ya wananchi kutembea vifua mbele kuwa wao ni CCM damu, ili hali viongozi wa ngazi za juu wa chama hicho ndio wanaofaidi.

Naye Makumu Mwenyekiti BAVICHA Taifa, Patrick Ole Sosopi, alisema kuwa licha ya Tanzania kuwa na rasilimali nyingi, bado ni masikini kutokana na viongozi wengi waliopewa dhamana ya uongozi kuwa wabinafsi.

Makumu huyo, alisema kutokana na viongozi wengi kuwa wabinafsi na muda wote wanawaza uchaguzi, wanakosa nafasi ya kuwatumikia wananchi na kwamba Tanzania inashindwa kupiga hatua kutokana na watu waliopewa dhamani kutokuwa na uchungu na taifa hili.

“Ndugu zangu Wanaipinda na Kyela kwa ujumla, nchi hii haipigi hatua kimaendeleo kwani watu tuliowapa dhamana si viongozi bali ni madalali ambao wanawaza familia zao tu na ili kuondoka na watu hawa niwaombe likianza zoezi la uandikishaji katika daftari kudumu, mjitokeze kwa wingi ili mshiriki vyema uchaguzi wa Serikali za mitaa kwa maana ya wenyeviti wa vitongoji,vijiji na mitaa na uchaguzi mkuu mwakani.

Aidha katika hatua nyingine, Sosopi alisema viongozi wa CCM chini ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta wameingia katika historia ya ajabu kwa kuruhusu marehemu kupiga kura kupitisha Katiba inayopendekezwa.

“Samwel Sitta na wenzake wanajitapa kwamba Katiba hii ni ya kihistoria. Hii ni sahihi kwani hakuna popote duniani isipo kuwa Tanzania tu ambapo hata marehemu wanapiga kura kupitisha Katiba wakati wa kutafuta theruthi mbili ili kuungwa mkono,” aliongeza Sosopi.

Aliwataka wananchi hao kuiadabisha CCM wakati wa kura za maoni kupitisha Katiba, inayotarajiwa kufanyika Aprili mwakani.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment