photo tyyyyyyyyyyyyyyyy_zpsd20272cf.jpg

NYALANDU AWASHANGAA WANAOTAKA URAIS.

WAKATI joto la Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani kwa mwaka kesho likizidi kupanda, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu amewashangaa wanaojitokeza kutangaza nia ya kuwania Urais, akisema nafasi hiyo ni nyeti ambayo wengi wanapaswa kuogopa kutangaza kuitaka.

Badala yake, ameshauri wasubiri wafuatwe na watu wenye `kuona mbali’ kwa lengo la kuwashawishi kuwania nafasi hiyo.

“Hapo zamani kuna kikao kilikaa watu wakasema na tumuumbe mtu kwa sura na mfano wetu. Na baadaye kikao kikakaa tena wajumbe wakasema tumtume nani…ndivyo inavyopaswa kuwa kwa nafasi ya Rais wa nchi pia,” alisema Nyalandu akiwa mjini hapa.

Alisisitiza kuwa, nafasi ya urais ni kubwa sana hivyo yeye binafsi hawezi kujitangazia nia ya kuwania nafasi hiyo na kuwabeza wachache wanaojitangaza akisema wanafanya makosa.

Alisema kwa uzito wa nafasi ya urais mtu hawezi kuibuka na kujitangazia kuitaka nafasi hiyo, bali anapaswa asubiri kushawishiwa na watu wengine watakaomwona anafaa kuwaongoza na kuwaletea maendeleo.

Nyalandu hakuweka wazi iwapo atagombea au hatogombea, lakini aliendelea kusisitiza kuwa watu wanapaswa kusema na si mtu binafsi kujisemea.

Aliwataka Watanzania kuendelea kumwomba Mwenyezi Mungu ili aweze kuwachagulia Rais atakayekuwa msikivu, mwelewa na mwenye kutambua umuhimu wa kuwajali watu anaowaongoza.

Wakati Nyalandu akiyasema hayo, watu kadhaa kutoka ndani ya chama tawala, CCM wameshaelezea nia yao ya kutaka kuwania urais mwaka kesho, akiwemo Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kigwangalla.

Wengine wanaotajwatajwa kwa nafasi hiyo na hata kujikuta wakiingia matatani na chama chao kilichowaita na kuwaonya kutojiingiza katika harakati zozote za kuwania nafasi ya chama hicho hadi muda mwafaka utakapofika ni mawaziri wakuu wastaafu, Frederick Sumaye na Edward Lowassa.

Wamo pia Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Sera na Uratibu, Stephen Wasira.

Akizungumzia tuhuma ambazo amekuwa akitupiwa kupitia gazeti moja la hapa nchini, Nyalandu aliendelea kusisitiza kuwa gazeti hilo linatumiwa na wahusika wa ujangili ili liweze kumchafua na kuondolewa katika nafasi hiyo.

Alisema anaamini utendaji kazi wake mzuri ndiyo sababu hasa ya gazeti hilo kutumika kumchafua kwakuwa anaonekana kuziba mianya ya ujangili waliyokuwa wakiitumia kabla ya yeye kuteuliwa kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii.

Nyalandu alisisitiza kuwa hatorudi nyuma katika kupigana vita ya ujangili hususani wa kuua tembo na badala yake atazidi kuweka mikakati yenye kulenga kulinda maslahi ya Taifa.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment