photo tyyyyyyyyyyyyyyyy_zpsd20272cf.jpg

CHINA YAMWAGA NEEMA KWA TANZANIA.

SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China imetangaza neema kubwa kwa Tanzania, ikiwa ni pamoja na kutoa dola za Marekani milioni 85 (Sh bilioni 140) kwa ajili ya shughuli za maendeleo na kuisaidia Tanzania kufanya mageuzi ya viwanda.

Neema hiyo ya China kwa Tanzania imetangazwa na Rais Xi Jinping wa nchi hiyo katika mazungumzo rasmi ya kiserikali kati yake na ujumbe wa Tanzania, ukiongozwa na Rais Jakaya Kikwete, ambaye yuko katika ziara rasmi ya siku sita nchini China.

Mazungumzo hayo kwenye Jumba la The Great Hall of the People, yalifanyika baada ya Rais Kikwete kukaribishwa rasmi katika Jamhuri ya Watu wa China kwa kupokelewa na Rais Xi Jinping katika eneo la East Plaza la Jumba hilo.

Katika mapokezi hayo, Rais Kikwete alipigiwa mizinga 21 na kukagua gwaride la ukakamavu la Jeshi la Ukombozi la Wananchi wa China.

Katika mazungumzo hayo, Rais Xi Jinping alitangaza kuwa China itaipatia Tanzania kiasi cha dola za Marekani milioni 85 (Sh bilioni 140), ikiwa ni mchanganyiko wa msaada na mkopo usiokuwa na riba, fedha ambazo Tanzania itaamua yenyewe jinsi gani ya kuzitumia.

“Katika kuunga mkono jitihada za Serikali ya Tanzania kuboresha maisha ya wananchi wake, napenda kutangaza kuwa China itatoa kiasi cha RMB milioni 200 ikiwa ni msaada na RMB milioni 200 nyingine zikiwa ni mkopo usiokuwa na riba kwa Tanzania.” “… na kiasi cha RMB milioni 100 za msaada kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambazo zitatumika kwa kadri Serikali hizo mbili zitakavyoamua,” alisema Rais Jinping.

Rais huyo wa China pia alitangaza kuwa nchi hiyo, itaisaidia Tanzania katika uendelezaji wa maeneo ya uwekezaji ya EPZ, uendelezaji wa miundombinu, itaharakisha ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo na itaingia katika shughuli za kutafuta gesi na mafuta katika ukanda wa Bahari ya Hindi katika eneo la Tanzania.

Rais Jinping pia alitangaza kuwa Serikali ya China imefanya uamuzi wa kuikarabati Reli ya TAZARA, inayounganisha Tanzania na Zambia na yenye urefu wa kilomita 1,860 na kusaidia uendeshaji wa reli hiyo.

“Ili kutekeleza uamuzi huu kwa haraka, napendekeza kuundwa kwa kamati ya pamoja ya wataalamu kuandaa ramani ya namna ya kuitoa reli hiyo katika matatizo yake ya sasa,” alisema.

TAZARA ndiyo reli ya kwanza duniani kujengwa na Jamhuri ya Watu wa China, ambao utaalamu wake sasa unasakwa na nchi nyingine nyingi duniani.

Rais Jinping pia alitangaza Serikali yake itatoa nafasi 100 za masomo ya elimu ya juu kwa wanafunzi kutoka Tanzania katika miaka mitano ijayo, itaongeza idadi ya madaktari ambao China inapeleka Tanzania, itahimiza kampuni zaidi ya China kuwekeza katika Uchumi wa Tanzania na kuzishawishi taasisi za kifedha za China kuanzisha shughuli zake katika Tanzania.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment