photo tyyyyyyyyyyyyyyyy_zpsd20272cf.jpg

KAMATI YA ZITTO YAWATIMUA MAOFISA WIZARA YA KILIMO.

KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imewafukuza kwenye kikao timu ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika iliyoongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo,Sophia Kaduma na kuipa wiki mbili kutekeleza maagizo kisha kuifuata kamati hiyo mjini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Kabwe Zitto, alitoa uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam mara baada ya timu hiyo kujitambulisha mbele ya kamati na kisha kutoa ufafanuzi wa baadhi ya mambo, ambapo majibu yake hayakuiridhisha kamati.

“Leo tunawarudisha hatukagui mahesabu yenu, jipangeni upya mtufuate Dodoma baada ya wiki mbili mje na mikakati inayotekelezeka,’’ alisema Zitto.

Maagizo waliyopewa wizara hiyo wayafanyie kazi na kupeleka majibu baada ya wiki mbili mjini Dodoma ni kuandaa mkakati unaotekelezeka wa kununua mazao ya wakulima, ambapo kwa msimu huu wa mavuno, mazao ni mengi na hakuna masoko.

Agizo la pili wanalotakiwa kulitekeleza na kulipeleka Dodoma ni kuwa na taarifa inayoonesha jinsi deni la Sh bilioni 3.8 la Kampuni ya Mbolea ya Minjingu linavyolipwa.

“Mikakati yenu haitoshelezi, haina msaada kwa mkulima ni sawa na serikali imewaacha wahangaike wenyewe, mahindi ni mengi hakuna soko, sasa kama hakuna ufumbuzi ni kuwaonea wakulima, ondokeni mkajipange mje na mkakati wa kununua mahindi ya wakulima kwa msimu huu,’’ alisema Zitto.

Alisema wamewarudisha wizara hiyo ili wakajipange na kisha waifuate kamati hiyo mjini Dodoma, baada ya wiki mbili wakiwa na mkakati huo kwani kuna ziada ya tani milioni mbili za mahindi kwa wakulima ambazo hazijulikani soko litapatikana wapi.

Awali, Zitto alimtaka Katibu Mkuu huyo kuonesha ni hatua gani wizara imechukua kuhusu ziada ya mazao yaliyozalishwa na wakulima katika msimu huu, ambapo mahindi ni mengi na soko hakuna.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment